Sunday, November 18, 2007

Fumbo, kitendawili na hadithi pamoja?


Mheshimiwa Zitto Kabwe

Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza rais Jakaya Kikwete kwa uamuzi wake wa kuunda tume ya kuchunguza suala zima la mikataba ya madini nchini, na napenda ifahamike kuwa pongezi hizi ni za dhati kwa maana ya kutoka moyoni, tena kule kilindini. Pongezi hizi ni kwa sababu mbili.

Kwanza ni kwa sababu ya rais kutimiza ahadi aliyoahidi hivi karibuni katika mkutano mkuu wa CCM pale Dodoma , aliahidi kufanya hivyo, naam amefanya tena kwa muda mfupi sana , ametimiza ahadi.

Lakini la pili lililokubwa zaidi ni kwa vile rais anaelekea kupona ule ugunjwa wa siku nyingi wa serikali ya CCM kufanya mambo kwa kuzingatia maslahi ya chama zaidi kuliko Taifa, uginjwa wa kudhani wapinzani hawawezi kutoa mchango wowote kwa serikali iliyoko madarakani zaidi ya kupiga kelele za majukwaani na kupoteza muda, hiyo ndio ilikuwa pengine ni dhana ya CCM na serikali kwa ujumla.

Lakini Kikwete ananishawishi nianze kuamini kuwa CCM ( kama si dhamira binafsi ya Kikwete) inaelekea kupona uginjwa huu, ni pale alipoamua kuunda tume inayojumuisha viongozi wa CCM na wale wa upinzani wakiwamo John Momose Cheyo wa UDP na Zito Zuberi Kabwe wa CHADEMA. Kwa moyo mkunjufu nasema hongera sana Mheshimiwa rais na asante !

Hata hivyo mwishoni mwa makala hii nitakutaka mpendwa msomaji wangu uamue/upembue uteuzi huu, ikiwa ni fumbo, kitendawili au hadithi kwa maana ya historia mpya ambayo vizazi vitasimuliwa hapo baadae?

Tume hii imekuwa gumzo mitaani na hasa kwa wafuatiliaji wa masuala mbalimbali hapa nchini, na aliyesababisha gumzo hilo si mwingine ni Zitto Kabwe, suala sio tume, suala ni Kabwe kuwa kwenye tume hiyo. Wakati gumzo hilo likiwa bado bichi, gazeti moja likaripoti kuwa baadhi ya wanachama wa CHADEMA wamanza kumjadili Kabwe, kwamba inakuwaje awe kwenye tume hiyo na mambo mengine mengi ambayo nimeyatafsiri kama ya kitoto kama sio propaganda za baadhi ya maadui wa Zitto Kabwe kupitia magazeti hayo. Suala la Zitto kabwe kuwa kwenye tume hiyo siyo suala la kiitikadi, ni swala la kitaifa.

Mimi sijui kwa upande wako unafikiriaje, wenzako wanasema Zitto Kabwe ana ajenda ya siri na CCM, kwamba ananunuliwa ili kuzibwa midomo, mimi nayakataa madai haya kwa nguvu zote, ni utoto wa kimawazo kuanza kufikiri hivi mapema, tusiache kujadili hoja ya msingi, tukianza kujadili uhalali wa Kabwe kuchaguliwa na rais anayetokea CCM tutawapa walfi nafasi ya kupumua kama wapo.

Na hapa leo nataka nikutafakarishe wewe mwenye mawazo hayo ya kitoto kuhusiana na uwepo wa Kabwe kwenye tume ya rais.

Unakumbuka kuwa Zitto Kabwe alifungiwa na Bunge (spika?) kuhudhuria vikao vya bunge kwa madai ya kulidanganya bunge, kwamba alitoa madai ya uongo, wengine wakafika mbali kwamba amemdhalilisha Waziri Karamagi? Unafikiri hii ina maana gain? Sikiliza wewe! tungeweza kumwita Kabwe ni mhalifu aliyeko kifungoni, lakini mpaka anatoka bungeni alisisitiza kuwa madai yake yalikuwa kweli, na akasema anawaachia wananchi wengine waamue, kwamba yeye alikuwa amemaliza zamu yake. Bunge likazodolewa na kushutumiwa na wanasiasa, wanaharakati na wananchi wengine wa kawaida. Ninakumbuka wakati ule nilikuwa Mbeya, nilipigiwa simu na mwanafunzi mmoja wa sekondari iliyoko Morogoro, huyu msichana alisema hivi, “niliiheshimu sana CCM, lakini sasa kwa hatua ya Bunge kumfungia Zito Kabwe, mh, mimi nahamia CHADEMA” Nilichomshauri ni kutulia ili afanye maamuzi sahihi, kuhama chama kusingemnusuru Zitto Kabwe wakati ule.

Zitto Kabwe aliitwa muongo, mzushi, wakasema anajitafutia umaarufu kwa kusema uongo, mjidala hiyo ikafika hata vyuoni na kuwagawa wanafunzi, wengine wakimtetea huku wengine wakimshutumu na kumwita kimbelembele, Zitto akasonga mbele, vyama vya upinzani vikachochea moto kwa kuamua kupanga ziara za kwenda kuishitaki serikali kwa umma, maana bunge lilishindwa kuidhiti serikali.

Mbele ya macho ya bunge Kabwe alikuwa ni mhalifu aliyeko kifungoni, kadhalika mbele ya Karamagi na Kikwete na baadhi ya wana CCM, sina shaka kwamba adhabu ya bunge kwa Zitto ilimfariji sana Karamagi aliyemwita Zitto Kabwe kuwa ni muongo na mdhalilishaji.

Wiki iliyopita limetokea jambo, sijui mpaka saa niliiteje, ninakupa nafasi ya kutoa jina. ‘Mhalifu’ yule yule, muongo, mzushi na mdhalilishaji aliyefungiwa kwa misimamo yake kwenye kulinda rasilimali za Taifa na hasa madini, leo amekuwa wa maana mbele ya rais hata kupewa ujumbe katika tume yenye kazi ya kuchunguza suala lile lile la madini. Unasemaje? Je, rais kapitiwa au anajua kwa hakika alichokifanya? Hajui kuwa Zito ni mfungwa? tena kwa sababu ya kutetea madini ya nchi yetu, madini ambayo yamefanya serikali ipoeze imani kwa wananchi wake? Rais amesahau kuwa waziri wake (Karamagi) anamchukulia kuwa Zito Kabwe ni muongo na mzushi? Kwa nini kaamua kumteua? Je, Zitto Kabwe ni msafi tofauti na anavyoonekana mbele za macho ya bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania ?

Je Zito Kabwe ni mkweli tofauti na fikra za Karamagi? Au kwa nini rais amemteua? Kwetu tunaamini kuwa mheshimiwa rais kazingatia na kuamini kuwa Zito Kabwe anafaa na anaiweza kazi aliyompa, kigezo cha uadilifu, uchapa kazi, ukweli na uwazi ndicho kilichompa kibali zito mbele za rais Kikwete.

Kama ndivyo basi, tuiteje uteuzi huo, ni fumbo la rais kwa Karamagi na bunge? Kwa maana kwamba bunge na Karamagi walivyomfikiria Zitto Kabwe sivyo alivyo? Au ni vipi? Kama ndivyo, je rais amemsuta Karamagi? Kwa hiyo kama ni hivyo, huo si ushindi wa kishindo kwa Zitto Kabwe kama mwanaharakati, kwamba sasa imethibitika kuwa alikuwa ni Nabii asiyeheshimika na kutiliwa mashaka bure tu!

Je hatuwezi kufikiri kuwa CCM na serikali yake imejizodoa? Mimi huko simo, ni katika kujaribu kuwaza na kuwazua, lakini pongezi zangu kwa rais zinabaki palepale!
Ni vipi pia? Uteuzi huo ni kitendawili? Nani atakitegua? Kinasemaje hicho kitendawili? Je ni hadithi mpya katika historia ya Tanzania ?

Suala la Zito kwenye tume hiyo limenikumbusha habari za RADA, wanaharakati walipotuhumu kuwa ina mazingira ya rushwa, baadhi ya wanunuzi wakapinga kwamba sivyo ilivyokuwa. Leo TAKUKURU imemtangaza mmoja wa watuhumiwa hao wa rushwa hadharani, hii ina maana kuwa mazingira ya rushwa yalikuwapo, je wanasemaje wanaposikia kuwa madai ya wale walioitwa wazushi yamethibitika kuwa na ukweli?

Naamini hili ni funzo hata kama rais amefanya bila kujua kuwa kuna watu wangekuja na tafsiri nyingi sana baada ya uteuzi huo.Kwa hiyo tunashawishika kuamini kwamba, kumbe kuna madai mengi ya wapinzani yakiwemo yale ya ufisadi tutakuja kuujua ukweli wake siku moja, tena watakaokuja kuuthibitisha ni hao hao wahusika, tuombe Mungu!

Kila la Heri tume ya rais!