Thursday, May 31, 2007

JE CCM, NI MASHETANI?


Mwasisi wa TANU na CCM, hayati Julius Kambarage Nyerere, akiwa na mkewe huko mahali fulani hivi!
JE CCM NI MASHETANI?

Nimekutana na mheshimiwa Fulani hivi karibuni, huyu nilipata fursa ya kujadili naye mambo yanayoihusu nchi hii na hasa siasa. Kumbuka niliwahi kukuambia kuwa napenda sana kila ninapopata fursa ninaijadili nchi hii.

Simuiti mheshimiwa kwa kumdhihaki, kwangu huyu ni mheshimiwa hasa, kwa sababu namheshimu kwelikweli, namheshimu kwa mambo mengi, ikiwa ni pamoja na mchango wake kwangu, kufikia hatua hii ya uandishi (sio uhandisi) wa makala gazetini na kwenye blogu.

Katika kujadili naye, bila kutarajia tukajikuta tayari tunazungumzia juu ya mfumo wa vyama vingi vya siasa hapa nchini. Na kwa kufupisha mada hii, nikuambie tu kitu ambacho huyu mheshimiwa alikisema. Yeye anasema na kuamini kua mfumo wa vyama vingi vya siasa ni ushetani, yaani asili yake ni uasi alio ufanya shetani kwa Mungu. Kwamba upinzani ni roho ya ushetani inayofuatilia na kufanya kazi katika mfumo huo. Wewe msomaji unasemaje?

Mwenzako huyu alianza mbali, anasema eti shetani kabla hajawa shetani alikua chini ya utawala wa Mungu. Kwamba alipotaka kuwa juu ya Mungu au kwamba hakufurahia kuwa chini ya utawala wa Mungu, akaamua kuanzisha kampeni za kumpindua Mungu. Hapo ndipo alipolaaniwa na kutupwa chini (duniani) ambako laana ile bado inaambukizwa kwa wengine wakiwemo wanasiasa.

Kwamba CCM ndio wamekua watawala wa nchi hii, na viongozi wa vyama vya upinzani hasa wale waasisi wanaendeleza mfumo wa kishetani, hii ndio kusema kwamba waasisi kama vile Mabere Nyaucho Marando wa NCCR-MAGEUZI, Abdallah Fundikira wa CUF na wengine wengi unaowajua ni walaaniwa. Pengine Fundikira anehesabika kama ‘mtakatifu’ maana ametubu dhambi yake ya uasi na kurudi nyumbani kwa watawala, yaani CCM. Lakini dhambi hiyo ya Fundikira na wengine wapotevu wameitubia wapi? Maana CCm si miungu wale, maana nao bila shaka wana mengi ya kutubu. Hebu tuachane na hayo badala yake turudi kwenye mada na tuchimbe kwa ufupi historia.

Ni muhimu kukumbuka kuwa, tunapoizungumzia CCM, tunazungumzia mtoto aliyezaliwa mnamo mwaka 1977. Alizaliwa na wazazi wawili waitwao Afro Shiraz Party (ASP) na Tanganyika African Union (TANU) Sijui nani kati ya wazazi hawa alikua mama na mwingine alikua baba, maana majina yao hayaonyeshi jinsia!

Huyu mtoto yaani CCM, alizaliwa na wazazi ambao kila mmoja ana asili yake. TANU kwao ni Bara na ASP kwao ni kuleeee visiwani. ASP akiwa kwao alikua chini ya mtawala mwarabu, ukipenda mwite Sultani. ASP akakua, baadae akaona mwarabu anafaidi sana akitawala visiwa vya Pemba na Unguja (Zanzibar) akaanza mapambano ya kumng’oa mtawala wake. Sijui ni kwa sababu ya uzee, Sultani akashindwa mapambano.

Haya tuendelee, TANU naye kwao walikua chini ya mtawala Mwingereza, naye roho ikaota kutu, wakajisikia vibaya kuona Mwingereza anakula nchi, wakaona anafaiiiiiiidiii kukalia Tanganyika, aeti wakaanza kudai kujitawala wenyewe! Wakafunga safari mpaka Umoja wa Mataifa – New York kuwashitaki Waingereza (watawala wao)

Sasa niambie hawa wazazi wa CCM tunawapa jina gain kwa mujibu wa yule mheshimiwa? Bila shaka ni waasi, wameasi watwala wao, ni kama vile shetani alivyotaka kumpindua anayestahili kile kiti cha Enzi, YEHOVA Mungu Mkuu! Kwa kusema hivyo basi ni walaaniwa? (nauliza) Kwa yeyote anayeamini kama yule mheshimiwa anavyoamini hawezi kujizuia kuamini kuwa TANU na ASP walifuatiliwa na ile laana ya Ibilisi. Na kwa sababu walikuwa wapinzani wa watwala wao, serikali zilizokuwapo madarakani kwa wakati huo, basi hawawezi kukwepa kuitwa mashetani.

Kwa bahati mbaya au nzuri sana, wale wazee, yaani ASP na TANU hawapo tena, lakini hawakuwa wagumba, walibahatika kuacha mtoto mmoja wakamwita CCM. Na kwa kua mtoto wa nyoka ni nyoka tutaepukaje kuamini kuwa mtoto wa shetani ni shetani, tutachekwa tukisema mtoto wa shetani ni kuku au samaki kwa kutaka kulazimisha watu kuamini yale tunayoamini sisi hata kama kwao ni sumu. Kwa hiyo hoja yangu hapa ni kwamba kama kuna watu wachache, kwa maslahi yao binafsi wnataka kupotosha umma kuwa upinzani ni ushetani hawajui kuwa anatushawishi sisi wengine na kutufumbua macho, na kutufichulia siri iliyofichika kwamba CCM ni ushetani uliokubuhu, ushetani uliokomaa, maana ni tangu wazazi wake TANU na ASP, ndiyo! Si waliwapinga watawala wao, waliwapindua! Pengine CCM bara watakua na la kujitetea, hivi kule visiwani CCM inaweza ikasimama kama mkereketwa huyu mmoja anavyoweza kusimama kuwa upinzani ni ushetani? Eti kwa sababu tu wanakipinga chama tawala? Je wanaweza kuepuka kuitwa mashetani baada ya wao kumpindua mtawala wao Sultani?

Mimi sitaki kuamini hivyo, lakini huwezi kunizuia kuamini kuwa, ikiwa vyama vya upinzani ni ushetani basi asili yake ni CCM.

Nitumie fursa hii kuwaomba baadhi ya wanachama, wapenzi, viongozi na wakereketwa wa chama cha mapinduzi, ambao hawafurahii uwepo wa vyama vya upinzani bila kujua umuhimu wake, kwamba wasijaribu kuupotosha umma kwa namna yoyote iwayo. Wapambane kwa hoja na si kuwatisha wananchi. Pengine yule aliyeibua mjadala huu hana cheo chochote ndani ya chama hicho, kiasi cha kwamba anaweza akasambaza upotofu huo. Lakini si ajabu kesho huyu jamaa atapewa uongozi wa ngazi yoyote katika chama hicho, na huku bado akiwa na chuki na vyama hivi, bila shaka utakuwa wakati muafaka wa yeye kutisha wananchi.

Nimeona niiseme mapema maana si ajabu, kuna watu wanauchukulia upinzani kama utapeli, wizi na propaganda, kama Shahibu Akwilombe, naibu katibu mkuu wa CHADEMA alivyosema mjini Tanga hivi karibuni.

Ninawaomba wanasiasa watumie majukwaa yao vizuri na hasa CCM. Hatuwezi kamwe kubeza ukweli kwamba kunaweza tokea siku ambayo CCM itaitwa chama cha upinzani. Kwa kuhofia hilo, tusitumie mbinu chafu kuwazuia raia kuwa wanachama wa vyama wanavyovipenda. Kwamba kuwatisha kuwa upinzani ni ushetani ni dhambi, kuwaambia vyama vya upinzani vina matatizo si haki, maana hakuna chama kisicho na matatizo, nasema hakunaaa!!

Nashauri kwamba kusitumike mbinu chafu kudhoofisha upinzani nchini, mchango wake ni mkubwa kwa maendeleo ya nchi hii, hata kama hawatakuwa watawala wan chi hii. Wacha kuwepo na ushindani wa halali, tabia ya kuwarubuni na kuwanunua viongozi na wanachama wa vyama vingine ni dalili tosha za kuisha kwa enzi za chama husika. Kama kweli kuna pesa zinatumika kuwahonga na kuwanunua wapinzani, bai hakuna tena demokrasia ya kweli katika nchi hii, na tu wadhambi hata mbele za Mungu na wadanganyifu kwa jamii ya kimataifa.

Najua ukweli huu si kila mwanasiasa ataufurahia, lakini kwa kweli hatuna jinsi, ni lazima tuukubali. Nasema hivi kama wana CCM wanaitakia mema nchi hii hawana budi kuacha mtindo wa kuwarubuni na kuwatolea mijicho wapinzani na kuwashawsihi kurudi huko. Tabia hii haitaigharimu CCM kwa upande wa maslahi, itatugharimu watanzania hasa wa nyonge.

Kwa nini? CCM ikae ikijua kuwa itakapokuwa madarakani kama chama pekee cha siasa nchini, ni wazi kwamba italewa, itajaa kiburi na kuzalisha udikteta ambao ndio ule nasema utatugharimu watanzania. Nani atakua na ujasiri wa kuizodoa CCM ndani ya CCM, leo tunao wakina Mtikila, Mbowe, Mbatia na wengine wengi kwa sababu wako nje ya CCM. Huko wangeambiwa wangoje vikao, vikao saa ngapi wakati nchi inaharibika? Vikao vipi wakati wanyonge wanazidi kudidimizwa?

Ujasiri wa kina Mbowe na wenzake unatokana na kwamba hakuna kamati yoyote ya CCM itakayomwita kumhoji kama mwanachama wake, aliyesemea mambo ya chama nje ya chama. Ndio hapa tunauona umuhimu wa vyama vingi nchini, na hili ndilo somo wanalopaswa kulijua watanzania walioanza kulishwa kasumba kwamba upinzania ni ushetani!

Najaribu kuwaza, kama kweli James Mbatia ndiye alitoa wazo la kuanzisha mfuko wa elimu nchini na ukaanzishwa, je ingekuaje kama asingekuwa mpinzani? Je angesikilizwa ndani ya CCM? Hilo ni swali, jibu lake sote tushirikiane kulitafuta kama tunadhani litatusaidia.

Pia nawaza (pengine kipuuzi) kwamba kama upinzani usingekuwepo nchini, hii nchi ingekuwaje kiuchumi na kisiasa? Jaribu kufikiri haya mambo, usiyachukulie kirahisi. Fikiria tu siasa za Tanzania zilivyo sasa, hasa kwa upande wa demokrasia, angalia hali ya uchumi wa nchi hii, fikiria wapinzania wasingekuwa wanafanya vitu ambavyo Makamba anaviita kelele za mlango au za chura, fikiria tu, pembua katika mawazo, usimjibu mtu, jijibu mwenyewe, kwa mtazamo wako, ijibu nafsi yako, uwe shahidi wa wewe mwenyewe, jiambie ukweli, hii nchi ingekuwaje?

Maneno ya kejeli kama ya Makamba na wana CCM wengine ukitafakari sana utakuta ni hofu tu iliyojengeka. We angalia watu wanapopigana kwa kutumia mikono (ngumi) mmoja anapozidiwa utakuta si ajabu akaamua kutumia silaha kinyume cha utaratibu kwa lengo tu la kujihami na kumshinda mpinzani wake. Hatutaki wana CCM wafike huko, na wapambane kihalali kabisa na wapinzani wao kisiasa. Kudai kuwa CCM ni ushetani hayo ni matumizi ya silaha haramu kwa kujihami. Haikubaliki hata kidogo!

Hebu fikiria! Je ni ushetani kwa mtu kudai haki yake na ya mwingine? Ni ushetani kuandamana kupinga maamuzi yasiyofaa ya serikali? Ni ushetani kudai marekebisho ya katiba inayojichanganya? Katiba inayozungumzia nchi ya ujamaa na hali ujamaa haupo? Au bado kuna ujamaa hii nchi?

Kuna madai kuwa mara kadhaa CCM imeiba kura (haya ni madai ya wapinzani) CCM wamekuwa wakikanusha tuhuma hizo, lakini fikiria kuwa kweli wameiba lakini ni kwa vile tu mwanadamu hawezi kukiri kosa kirahisi wanakataa, sasa kama kweli waliiba, je huo si ushetani?

Hebu nisiwe kasuku hapa, tuonane wiki ijayo kwa neema ya Mungu!