Tuesday, May 29, 2007

Eti daladala zinakatisha ruti, mnamwambia nani maneno hayo?


Nasikia tunailalamikia serikali kuwa daladala zinakatisha ruti, eti kwamba hazifiki kule zilikopangiwa kufika ba hivyo kusababisha usumbufu kwa abiria. nataka nijue, wakati wanakatisha hizo ruti ninyi abiria mnakuwa wapi?
nauliza hivi si kwa nia ya kuwatetea watu wa daladala, isipokuwa nimegundua kuwa baadhi usumbufu mwingi tunaoupata wananchi wa Tanzania husababishwa na sisi wenyewe. Naongea hivi nikimaanisha sambamba na uchungu nilionao.
Hivi karibuni nilikuwa nasafiri kuelekea Tanga, gari (basi) tulilokuwa tumepanda lilijaza kiasi cha abiria wengine kusimama. Tulipofika kituo cha Kibaha, askari mmoja wa usalama barabarani alisimamisha lile gari na kulitaka kutoendelea na safari
Ndugu yangu kilichotokea kilinishangaza, abiria wakawa wanampinga yule trafiki kwa kitendo chake cha kuwashusha abiria waliozidi kinyume na sheria za usalama barabarani. Wakati huo siku chache zilizopita nilikuwa nimetoka kuzungmza na maofisa wa Wizara ya miundo mbinu kuhusu suala la abiria kupunguzwa na kukalia vigoda kwenye baadhi ya mabasi ya mikoani.