Saturday, July 21, 2007

Happy Birthday Madiba

Nelson Rolihlahla Madiba Mandela

Naandika makala hii kwa heshima kubwa ya mwanaharakati chipukizi kabisa, mwanafunzi wa sekondari, Elizabeth David wa Arusha. Ni moja ya hazina zinazochipuka kwa taifa hili wakiwa na moyo wa uzalendo kwa Taifa hili, nikipata nafasi nitaeleza kirefu kuhusu yeye.

Leo namzungumzia Nelson Rolihlahla Madiba Mandela, kwangu huyu ni mmoja kati ya zawadi ambazo Mungu aliamua kuutunuku ulimwengu, namwita shujaa na hilo halihitaji ufafanuzi wala wakati wa mjadala. Maisha yake yanajieleza.

Alizaliwa kitongoji cha Transkei nchini Afrika ya Kusini tarehe 18, julai 1918, hii ina maana kwamba wiki iliyopita tarehe 18, jumatano mwana huyu wa Afrika alitimiza miaka 89. Kwa faida ya wasomaji wa safu hii, shujaa huyu alizaliwa na baba ambaye alikuwa chifu wa kabila la Watembu, aliitwa Henry mandela.

Miongoni mwa mambo mengi ambayo pengine wengi wetu hatuji labda kwa sababu hayajaripotiwa sana, ni kwamba kwa taaluma Mandela ni mwanasheria aliyehitimu shahada yake katika chuo kikuu cha Witwatersrand mwaka 1942 kabla hajawa mwanasiasa kwa kujiunga na ANC mwaka 1944

Kuishi maisha ya miaka 89 katika ulimwengu huu uliochanganyikwa si kitu kidogo hasa kwa mtu kama mandela aliyepitia karibu robo ya maisha yake. Kati ya misukosuko ikiwemo kuwekwa gerezani kwa miaka ipatayo 27.

Unaweza kumwita Mandela shujaa, jasiri, mapambanaji au mwanamapinduzi. Alipinga uonevu wa kila namna, alikataa ukandamizaji na aina ya maisha ya watu waliotaka kujifanya miungu wa dunia hii. Kwa nini nasema haya yote! Sikiliza mandela alivyosema mwenyewe:

Anasema “Nimepinga utawala wa watu weupe, nimepinga utawa wa watu weusi. Nimeheshimu mpango wa kidemokrasia na jamii iliyo huru ambapo watu wote wataishi pamoja kwa amani pamoja na fursa sawa. Ni mpango ambao nitaishi kwa ajili hiyo na kuufanikisha. Lakini ikibidi, basi ni mpango ambao nimejiandaa kufa kwa ajili yake”

Maneno haya ni mazito sana, Mandela aliyasema haya alipohukumiwa kifungo cha miaka mitano katika kesi fulani hivi, eti kwa kosa la uhaini, lakini uhaini uliodiwa na maadui zake ni kile kitendo cha yeye kupinga ubaguzi wa rangi nchini Afrika ya Kusini. Hiyo ni mwaka

Kwa wale amabo wamefuatilia maisha ya harakati ya Madiba wanaweza kukubaliana na mawazo yangu kwamba Mandela hakuwa tu msemaji bali pia mtu wa vitendo, na si hivyo tu bali pia alianza kutenda kabla ya kusema, upo hapoo? Baada ya kutafakari hayo, nikajikuta nakumbuka aya fulani ya Biblia inayosema “kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha” Matendo 1:1 Unaona hapo, watu wanaanza kutenda na kisha kusema au kufundisha.


Je wakoje wanasiasa wetu wa leo, unaweza kuwafananisha na Mandela? Je wanamfikia hata kwa mbali? Wangapi angalau wanatenda wanachokisema? Mandela alianza kutenda kabla hajasema, alianza kupigania uhuru wa waafrika hata kabla Afrika haijajua dhamiri yake, kabla waafrika hawajajua, kabla hatamka hadharani kuwa amejitolea maisha yake kuipigania Afrika!

Kwa nini nasema kuwa alianza kutenda kabla hajasema? Tuirejee kwanza sehemu ya kauli yake “Ni mpango ambao nitaishi kwa ajili hiyo na kuufanikisha. Lakini ikibidi, basi ni mpango ambao nimejiandaa kufa kwa ajili yake”

Angalia maisha yake kabla ya kuwekwa gerezani, alipigania uhuru wa weusi, kitu ambacho wazungu walikitafsiri kama uhaini na hivyo kumtupa lupango.

Je, alipigana kabla ya kutoa kauli hiyo gerezani?
Ndiyo, hii ni bada ya chama chake cha ANC kupigwa marufuku kuendelea kuwapo nchini Afrika ya Kusini mwaka 1960. Je Mandela akaishia hapa? Hapana, kitendo cha ANC kufungiwa kilichochea moto wa harakati za mandela kwani kwa ushawishi wake baadhi ya maodfisa wa ANC walikubali kuunda kikundi kingine cha harakati za ukombozi kilichojulikana kwa jina la Umkhonto we Sizwe kikiwa na malengo yale yale ya ANC, wao walikitafsiri kikundi hiki kama ubawa (wing) wa ANC. Kwa kitendo hicho, ilipofika mwaka 1962, Mandela alikamatwa na kuhukumiwa kifungo miaka mitano pamoja na kazi ngumu akiwa gerezani, hatia kubwa kwa mujibu wa wazungu ni kwamba, eti Mandela alikuwa akitaka kuipundua serikali yao nchini humo. Ndio maana nasema alianza kupambana kwa ajili ya ndugu zake waafrika, hata kabla hajawaambia kuwa atapambana kwa ajili yao! Tuko pamoja?

Mwaka 1964, July, 14, Mandela na wenzake walihukumiwa kifungo cha maisha. Kitendo hicho kilikuwa kama kinauamsha ulimwengu kuanza kujua hasa Mandela alikuwa nani kwa Waafrika.

Nelson Mandela aliachiwa huru februal 11, 1990 . Je aliacha kutekeleza ahadi yake kwa waafrika? Hapana kwani kwa moyo wake wote akajikita zaidi katika mapamano kama alivyokuwa ameahidi, alipigfania kutimiza ndoto zake. Ndoto gani? Alisema hivi “Nimepinga utawala wa watu weupe, nimepinga utawa wa watu weusi. Nimeheshimu mpango wa kidemokrasia na jamii iliyo huru ambapo watu wote wataishi pamoja kwa amani pamoja na fursa sawa. Ni mpango ambao nitaishi kwa ajili hiyo na kuufanikisha. Lakini ikibidi, basi ni mpango ambao nimejiandaa kufa kwa ajili yake”
Ndio maana mwaka 1991, katika kongamano la kwanza la ANC, Mandela alichaguliwa kuwa rais wa ANC huku swahiba wake Oliver Tambo akiwa Mwenyekiti.

Tangu wakati huo, Mandela hajaacha kupambana, wiki iliyopita huku akiadhimisha miaka 89 ya kuzaliwa kwake, alizindua kikundi cha viongozi mashuhuri, wazee wenye hekima duniani kikiwa na lengo la kutatua matatizo yanayoikabili dunia kwa sasa.n Kikundi hiki kikiongozwa na Mandela mwenyewe kwa kusaidiana na mkewe Graca Machel na mwenyekiti wake, Askofu mkuu mstaafu, Desmond Tutu watatumia hekima walizojaaliwa na mwenyezi Mungu kuikwamua dunia kutoka mahali pabaya ilipofika. Unaweza kuona sasa, kwamba Mandela bado anapambana.

Swali langu ni hili, je viongozi wetu wa leo watakuaje watakapofika umri huu wa Mandela? Je watakumbukwa na kuenziwa kama tunavyomuenzi mzee huyu? Mbona baadhi yao wameanza kuchokwa na watu wao, majimboni, wilayani, na kwinginekeo wakati hata miaka 60 bado? Hii ni changamoto, Mandela hajatumia uchawi, uchawi wake mkubwa ni moyo wake wa kujitoa kwa ajili ya watu wake, na wala sio kujaza matumbo tu kwa kula vya wananchi.

Nilikwambia naandika makala hii kwa heshima kubwa kabisa ya wanaharakati akiwemo binti mdogo Elizabeth David, je wao watakuwaje? Kwa mfano, Elizabeth anampend sana Mandela, basi ni vizuri akatamani pia moyo wa Mandela, ili afanikiwe na kisha kuenziwa baadae!

Nimalizie kwa kumtakia kila la heri, mzee Nelson Rolihlahla Madiba Mandela, heri yake ya siku ya kuzaliwa!

Wednesday, July 4, 2007

WARAKA WANGU KWA WATANZANIA!

Nianze kwanza kwa kukusalimu popote ulipo ee Mtanzania, poleni kwa yote ambayo mnakutana nayo katika kila iitwayo siku kwenu. Baada ya salamu napenda kuwauliza swali, je ninyi ni wazalendo? Tafadhali lifanyie kazi swali hili.

Baada ya swali hili naomba nitoe ombi langu kwako wewe uliyebahatika kusoma waraka huu. Chonde chonde, jitahidi, fanya kila uwezalo uhakikishe waraka huu unasomwa na watanzania wengi kama si wote. Jitahidi kuwa mbunifu ili kufanikisha hilo.

Unaweza ukanunua nakala nyingi kadri uwezavyo na kuwagawia watanzania wengine, (hakikisha unayempa ni mtanzania) Pia unaweza ukasoma na kuanza kuzungumza na wenzako kuhusu waraka huu, nenda kawaelimisha, usijali kama wataukubali au watakataa ujumbe huu! Omba tu wakupe nafasi wakusikilize.

Pia unaweza ukatuma anuani ya tovuti ilipo hapo juu kwa wote walioko mikoani na nje ya nchi, waambie wasome kupitia mtandao wa ‘Internet’ anuani yenyewe ni hii www.amkenitwende.blogspot.com, tafadhali nisaidie kuufikisha ujumbe huu kwa watanzania wa rika, hadhi, jinsia na hali zote, nisaidie tafadhali!

Kwa nini nimeamua kuandika waraka huu? Nimekuwa nikisisitiza kila siku kwamba hii nchi ni ya kwetu. Ni sisi ndio tutakaojenga au kubomoa nchi hii. Nchi hii si mali ya CHADEMA, CUF, CCM, UDP, NCCR-Mageuzi au vinginevyo. Hakuna waziri au Mbunge mwenye hati miliki ya nchi hii. Hata Mwl. Nyerere alikuja, akaitumikia nchi hii, kwa kutambua kuwa hii nchi si mali yake, ulipofika wakati akawaachia watanzania wengine kuongoza nchi hii.

Ninachosisitiza hapa ni kwamba hii nchi ni watanzania walioko kule Magila kule Gonja, ni wale walioko Mlalo, Lushoto, walioko Kizorogoto kule Morogoro na kila paitwapo Tanzania. Kuna haja ya kuondoa dhana ndani ya fikra zetu kwamba Tanzania inamilikiwa na SERIKALI, kwa hivyo wananchi wa kawaida hawana la kufanya katika kujenga nchi hii.

Nakumbuka siku moja nikiwa eneo mojawapo hapa Dar es salaam, katika mitaa ya eneo hilo ilijaa uchafu na madimbwi ambayo ulikuwepo uwezekano mkubwa na wa kutosha kabisa kuondosha ile hali. Ilinibidi kuzungumza na baadhi ya wakazi kuhusu suala la uchafu ule. Mmoja wapo alijibu na kusema kwamba sisi sio jiji, kuhusu kupasuka kwa mabomba yanayotoa maji na kumwaga barabarani walisema wao si DAWASCO hata waamue kushughulikia tatizo hilo.

Kwa watanzania wengi kila kitu kinafanywa na serikali, pengine enzi za ni athari za ujamaa ndizo zinazotusumbua kwa sasa, lakini je hii nchi bado ni ya kijamaa kwa kweli? Hata kama Katiba inaeleza hivyo katika kifungu cha………

Kila mwanadamu anayezaliwa katika ardhi hii huzaliwa kwa makusudi, na ndio maana ni vizuri kujihoji kila mara, UNAIFANYIA NINI TANZANIA? Naamini kwamba ni watanzania wengi sana hawajawahi na hawana mpango wa kujiuliza swali hili, kama imani yangu ni potofu naomba nisamehewe. Yote haya ni kwa sababu tunadhani hatuhusiki kwa namna yoyote katika kuijenga nchi hii, na ndio maana kila kinachotokea na kutudhuru hutupa lawama kwa serikali, lakini tunashindwa kukumbuka kuwa pengine tunahusika kuifanya serikali ifanye yale inayoyafanya.

Sikatai kuilaumu serikali, serikali ni mzazi, anabeba lawama pale anaposhindwa kuwafanyia watoto wake stahili yao. Lakini hatuwezi kumlaumu mzazi eti kwa sababu mtoto wake mwenye umri wa miaka 24. mwenye akili timamu, mwanafunzi wa chuo kikuu mwaka wa kwanza haogi kwa sababu ya uvivu tu! Hatuwezi, tutaonekana wehu!

Kama wananchi tuna wajibu wetu kuhakikisha nchi hii inakwenda kuliko inakotakiwa kwenda. Naomba nitoe mfano kidogo hapa.

Hivi karibuni kumetokea ajali za kutosha zilizo poeteza watanzania wenzetu, sasa hawapo, wamelala mauti! Hatukuchelewa baadhi yetu kuilaumu serikali kwa sababu ya ajali hizo. Moja ya sababu zilizotolewa na baadhi ya wahanga wa ajali hizo ni mwendo kasi! Hili nalo tumeilaumu serikali.

Kuna wakati tuliilaumu serikali kwa sababu ya magari kujaza abiria kwenye mabasi yaenadyo mikoani! Ngoja nkiupe kisa hiki halafu niendelee!

Tarehe 19/05/2007 nilisafiri kimasomo kwenda mkoani Tanga, kama kawaida nilipanda gari pele stendi kuu. Safari ilianza vizuri sana, lakini tulipofika kituo cha Kibaha, lile basi lilipakia abirai zaidi kiasi cha kufanya wengine kusimama, kumbuka hiyo ni safari ya kwenda Tanga.

Kitendo kile kilishuhudiwa na askari mmoja wa usalama barabarani ambaye alipanda lile gari na kuwataka abiria wengine wapungue. Ndugu yangu abiria waliokuwamo kwenye gari walikuja juu kwa kitendo cha yule askari kutaka kupunguza abiria. Hoja yao ilikuwa ni kwamba wanacheleweshwa. Sio siri nilishindwa kuvumilia kile kitendo cha abiria wenzangu.

Nilisimama na kumtetea yule askari, si kwamba nilikosa siti ya kukaa, nilikuwa nayo! nikawa kama nimewasha moto ndani ya basi, kwani abiria wote walikuja juu na kuniita mnafiki, nilikuwa katika wakati mgumu sana. Katika lile gari kulikuwamo mwanafunzi mwenzangu yeye anachukua masomo ya sheria. Akageuka na kuwa mwiba kwangu, yeye alivuka mipaka na kutaka kunivamia ili kunipiga mbele ya askari wapatao watatu pale Kibaha, huyu ndiye mwanasheria wan chi hii baadae! Hoja yake ni kwamba mimi ni kimbelembele na kwamba nachelewesha safari za watu!

Amini usiamini askari wote pale walizidiwa nguvu na abiria, gari ikaachwa iende ikiwa na abiria waliosimama kama mizigo kwenye basi. Na abiria wale waliapa kwamba nikipanda lile gari nitakiona cha moto, nakwambia nilishushwa na kutafutiwa gari ingine. Hii ndio nchi yetu, na wale ndio watanzania wenyewe. Ajali ingetokea pale, lawama ni serikali.

Hiyo ni moja, pili nakumbuka nilikupa kisa kimoja nilipokuwa natokea Nairobi kurudi nchini, kwamba gari ilikwenda mwendo wa kasi mno, lilikuwa ni basi la kampuni ya SABCO, wakati tunalalamika mwendo huo, kuna abiria wakatupinga vikali na kumtaka dereva aongeze mwendo zaidi. Mungu bariki tulipofika maeneo ya michungwani mkoani Tanga, askari mmoja alisimamisha liele basin a kumuonya yule dereva, kasha akatoa namba yake ya simu ikiwa yule dereva ataendesha kwa mwendo mbaya, si hivyo tu alituachia jina lake kuwa anaitwa YOHANA, Ee Mungu tupe askari wengine wengi kama Afande YOHANA!

Ndugu zangu sijasahu nilipokuwa mkoani Singida mwaka 2004 ambako nilikwenda kwa shughuli za kuhubiri ujumbe wa neno la Mungu, niligombana na baadhi ya wasafiri wenzangu kwa sababu ya kuzidisha abirai kwenye basi la kampuni ya TASHRIF, ambayo baadae ilipata ajali muda mfupi baada ya kuondoka Stendi kuu ya Singida.

Hivi una habari kuwa kuna watanzania huwa wanachanga pesa ili kuwalipa askari wa usalama barabarani pindi madereva wanapofanya makosa? Tunailamu serikali kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake kama yale ya kulinda usalama wa raia wake, je sisi tumetekeleza yapi ili kulinda usalama wetu? Pengine ni maneno magumu na machungu sana naongea hapa, mniwie radhi, nivumilieni, huu ndio ukweli!

Hii ninayoitoa hapa ni mifano kidogo tu! Watanzania tumekuwa pia na nidham ya uoga isiyo kifani, tuna chembe Fulani ya unafiki.

Siku moja tukiwa darasani chuoni, kulianza mjadala kuhusu tatizo la rushwa Tanzania, katika hali ya kustaajabisha kuna baadhi wakawa wanakiri na kusimamia kwamba rushwa haiwezi kuondoka, ungesikiliza kwa makini ungegundua kuwa si kwamba haiwezi kuisha kwa sababu ya ugumu wake, bali ni kwa sababu ya maslahi ya watu Fulani, kuna wajumbe wakafikia hatua ya kusema bila haya kwamba ihalalishwe! Hawa ni watanzania! Ninyi mnapigana na adui upande wa kusini, upande wa kasikazini kuna wapiganaji wenzetu wanamtia moyo adui na kumpa mbinu za kutushinda!

Makala hii itaendelea wiki ijayo!

Thursday, June 28, 2007

AMINA CHIFUPA, ALINISUTA!

Amina Hamis Chifupa, kama kweli amekufa, basi na tuyakubali matokeo! Lakini kama kuna mahali kafichwa Amina, ni maombi yangu kwa Mungu kwamba siku moja utaonekana na kufa tena kwa mapenzi ya Mungu!
Umenifundisha kwamba umuonavyo mtu sivyo alivyo, na kwamba tabia za mtu huweza kubadilika, kitu kimoja nitakukumbuka ni ujasiri wako na uchungu (kama ulitoka moyoni) juu ya maisha ya vijana yanayoharibiwa na dawa za kulevya!
AMINA HAMIS CHIFUPA




Je unaweza ukafikiri ni uchungu kiasi gani mama huyu amepata, angalia anavyolia, je unapata hisia yoyote hapa? Hamisha nafsi ungekuwa wewe ndiye huyu mama hapa! fikiria kupoteza binti mbichi kama Amina. Basi huyu ni mama yake Amina Chifupa Judy Mbaga, akilia kwa namna ambayo imezidi hata ule tunaoweza kuita ni uchungu, sijui tusemeje?

Kama kweli umekufa, Buriani!

Nasema kama kweli Amina kafa, basi nasema buriani, kama nitapata nafasi kuna siku nitakuambia ni kwa nini nahisi kuwa Amina hajafa! Akili yangu inakataa kuwa Amina Kafa, hata mimi sijui kwa nini, namuona Amina, lakini sijui yuko wapi, lakini kama kweli kafa basi BURIANI!
"Siku nikilala, lala mauti, hakuna awazeae kuniamsha
Ndugu na jamaa, watalia, lakini hata hivyo sitawasikia
Utakuwa mgeni wa nani, wakati kifo kikifika?"


Hili ni shairi la muimbaji wa nyimbo za Injili Tanzania, Epharaimu Mwansasu. Ni saa nne kasoro za usiku kwa saa za Afrika Mashariki, nimekaa nyumbani napitia magazeti. Mara simu yangu inaita, siijui namba hii wala hata kuikumbuka kama nimewahi kuitumia. Naipokea na yule mtu anauliza “aisee wewe ni Daniel Gingo” Kwanza napata mashaka, kwa sababu karibu kila siku baadhi ya watu wananitabiria kudhurika eti kwa sababu ya kuandika makala zinazoishambulia serikali, lakini baadae nikajibu kuwa mimi ndie, mara anasema “Amina Chifupa hatunaye”

Nikahisi kuwa masikio yananidanganya, nikauliza “unasemaje” kama sikosei nadhani yule mtu alinijibu hivi “ndio hivyo” Sikumbuki ni saa ngapi niliacha lile gazeti nililokuwa nalo, nikainuka kukimbilia chumbani ambako ndiko iliko maktaba yangu na kufungulia redio ili kujaribu kuthibitisha kifo hicho, hali ilikuwa tata, nikajikuta naishiwa nguvu, na hivyo kukaa kitandani kwa muda mrefu kidogo bila kujua nafanya nini.

Makala yangu ya mwisho kuandika kuhusu Amina ilikuwa ni juu ya tuhuma dhidi yake kuwa alikua na uhusiano na Mbunge mwenzake, Mheshimiwa Zitto Kabwe, katika masuala ya dini, tuhuma hizo huitwa uzinzi. Niliuandikia umma kwamba tusishangae Amina kuwa na tuhuma za jinsi hiyo, maana yeye nae ni mwandamu, haukna kunyoosheana vidole, maana uzinzi ni ugonjwa wa wengi, wakiwamo mashehe na maimu, mapadri na wachungaji. Nilisema uzinzi ni dhambi inayomnyemelea kila mmoja. Ni wajibu wa kila mmoja kujilinda! Baada ya taarifa za kifo chake kesho yake nilifungua Internet kwenye blogu yangu kuisoma tena ile makala na picha iliyopamba makala ile, kuna picha ya Amina alipokuwa akiapishwa bungeni.

Kitu ninachotaka kuandika hapa siandiki kwa sababu Amina amekufa, tumeshuhudia watu wengi wakimpa sifa Amina lakini ukiwatazama usoni ni unafiki umewajaa! Ni bora kuwa kimya, kuliko kuzungumza vitu vya kinafiki. Hata hivyo tumezoea hayo. Sifa alizopewa Amina utafikiri sio yule aliyekua akindikwa kwa kashfa kila kukicha magazetini!

Ninachandika hapa ni kutaka kuonesha kwamba mimi ni mmoja wa watu ambao marehemu Amina alitusuta, siko hapa kumpamba, niko hapa kueleza ninachokijua.

Wakati anaanza harakati zake za kuwania ubunge wa viti maalumu kupitia UVCC kuliibuka mijadala mitaani, kila mtu alisema lake. Mmoja kati ya watu ambao walipinga Amina kuwania kiti hicho kwa herufi kubwa ni MIMI. Tulibishana na watu japo wengi hawakuwa na hoja za kunishawaishi kwamba kwa nini Amina anafaa. Mimi nilikataa kwanza kwa sababu ya umri wa Amina wakati ule, akiwa na umri wa miaka 24, jambo la pili na kubwa ni zile habari zake za mitaani na magazetini.

Kama alivyosema Kulwa Mzee katika gazeti la Majira la Juni 28, 2007

“Umri wako(Amina Chifupa) mwanzo uliowagopesha watu(mimi ni mmoja wao) na kuwafanya wahisi kwamba hautaweza kufanya chochote bungeni lakini ulionesha maajabu kwa kuanza kushughulikia mambo ya msingi ambayo hata hao waliokuwa wakionekana kwamba ndio walistahili kufanya hivyo hawakuweza kufanya hivyo”

Kwa wakristo tunaamini kuwa imani yoyote huja kwa kusikia, kusikia na kusoma vyombo vya habari kulinifanya nijenge imani hasi kwa Amina hasa katika suala la yeye kuwa Mbunge. Niliamini na bado naamini kuwa nafasi hiyo ni nzito na yenye kuhitaji watu makini zaidi na wanaojua wanachokifanya!

Habari za Amina zilitawala zaidi magazeti yale yanayoitwa ya Udaku, habari zingine zilikuwa na ukweli mtupu ndani yake, maana mengine yalishuhudiwa mitaani na mengine kuendelea kufikirika na kudhanika.

Hisia zangu hasi hazikumzuia Amina kupata nafasi ya ubunge, alitinga bungeni, hata hivyo kuingia kwake bungeni bado hakukunifanya nifarijike na kuamini kua anaweza.

Amina alianza kunisuta kuwa imani zanguhazikua sahihi dhidi yake, ni pale alipoanza kutoa michango bungeni, alinimaliza na kunifunga mdomo kwenye suala la madawa ya kulevya. Hapo nikaanza kujua kua hisia zangu zilikua kweli lakini si sahihi (unataka ufafanuzi hapa?)

Suala la Amina kusiamama hadharani na kesema yuko tayari kutaja majina ya wahusika wakuu wa dawa za kulevya nchini, hata kama atakuwa ni mama yake ilikua ni kauli kali ambayo ingezungumzwa na mtu jasiri na mzalendo tu! Mtu aliyekubali kujitoa mhanga! Kauli hii bei yake ni ghari mno, wengi wameshindwa wakiwamo wabunge wa miaka nenda rudi kakatika bunge la Tanzania! Kauli hii haiwezi kutolewa na wabunge maslahi waliowadanganya wananchi kuwa watawawakilisha, kwamba watakua sauti zao, halafu wakafika na kupumbazwa na viti vizuri vya jumba la bunge na hata kufikia hatua ya kusinzia wakati wa vikao vinavyojadili mustakabali wa Watanzania walioko majimboni mwao.

Kitendo cha Amina kusimama kidete ndicho kilichonisuta mimi, narudia kusema kwamba sisemi haya kwa lengo la kutubu, sifanyi hivyo kwa sababu kwa wakati ule hisia zangu zilikuwa sahihi, kwanza sikuwahi kumuana Amina akiwa Mbunge (japo hili si zito sana)


Wachambuzi wengine wamesema, Amina alijitoa mhanga kupambana na watu hatari kwani wahusika wengi wa baishara hiyo ni watu wakubwa wakiwamo pia baadhi ya vigogo na wafanya biashara wakubwa ambao wako tayari kufanya lolote kwa yeyote yule anayekwamisha biashara hiyo.
Hili ndilo ninalo sisitiza kwamba limenisuta na kujifunza kwamba usiusemee moyo, kwangu Amina ni kama Anne Kilango Malecela, ikumbukwe hivi karibuni aliijia juu serikali kwa uamuzi wake wa kuachilia baadhi ya bidhaa kupita bila kukaguliwa. Kitendo cha Anne Kilango kimenifanya nimtazame kwa upya, nimuone kama mwanamke wa shoka. Imenifundisha kwamba kumbe wako watanzania wanaoweza kusimama kidete kutetea maslahi ya nchi hii bila kutetereka!

Kumbe wako wabunge wanaoweza kusema hapana kwa yale ambayo ni maovu na madhara kwa Taifa hili.

Kama kweli amekufa basi naomboleza kifo cha Amina kama mwanadamu yeyote, imeniuma kama ilivyoniuma kw mtu mwingine angekufa. Siwezi kumpongeza kwa sasa maana hayupo tena.

Nasema kama kweli amekufa basi, Amina amelala, Amina hawezi kuamka, amelala kama tutakavyolala wengi! Mitaani tayari kumeanza kusemwa mengi! Huko sitaki kujiingiza, ukweli unabaki kuwa Amina hatunaye tena.

Binti mdogo mwenye ndoto kubwa, aliyenisuta kuwa nilivyokua nikimdhania sivyo, nilikubali na kuanza kupata matumani kuwa sasa ataweza, ndio maana tukaamini kuwa anahitaji kuungwa mkono, ukiondoa kashfa za hapa na pale!

Kama mwanadamu naweza kusema kwamba, Amina ni miongoni mwa binadamu waliopitia misukosuko mingi katika maisha, kifamilia, kisiasa na kijamii kwa ujumla.

Sina namna nyingine ya kumpamba, kwa sababu sikua karibu naye, sitaki kujikosha kwa familia yake kwa kusema yale nisiyoyajua. Amina nilikuwa nikismsikia na kumsoma tu kwenye vyombo vya habari. Kama kweli amekufa basi salamu zangu za rambirambi ni kwa wanaharakati wote wa haki na usawa, wapiga vita wote wa kila aina ya uharamia duniani, najua tumepoteza kiungo! MUNGU ATUSAIDIE WOTE!


Saturday, June 23, 2007

Waraka wangu kwa Rais Kikwete!


Rais Jakaya Kikwete akionekana mwenye kuumiza kichwa kutafakari jambo fulani, hapa ni kama vile anasema "ama kweli kazi ninayo'

Ninakusalimu kwa heshima zote unazostahili mheshimiwa Rais upendwaye na wengi. Uniwie radhi sana ikiwa ninakukera kwa kutumia muda mwingi kuiandikia serikali yako. Hii imesababisha watu kuniuliza kwa nini kila makala ninayotoa huwa ‘naishambulia’ serikali. Mimi siishambulii serikali, kwa mtazamo wangu mimi naisaidia serikali kwa nafasi yangu niliyonayo.

Hata hivyo ikiwa mtu ataniuliza kwa nini naishambulia serikali, na ikiwa ni kweli nafanya hivyo, basi nitamjibu kuwa sina sioni sababu ya kutosihambulia! Kirahisi tu, nitajibu hivyo!

Mheshimiwa rais, nimewahi kuandika kuwa nchi hii ina rais mmoja tu, na kuwa rais haimaanishi kuwa unajua na kuweza kila kitu, nikasema, ndio maana unahitaji mawaziri, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na waandishi wa habari na wachambuzi kama sisi kukusaidia kutekeleza majukumu yako ya kila siku. Ka msingi ho usituchukie wala kutuwekea kinyongo eti kwa sababu tunakuandika kila mara!

Mara nyingi ninyi watu wa serikali mnapoandikwa kwa namna msivyopenda huwa mnalaumu vyombo vya habari na kushauri kuwa vitumie taaluma hiyo kuwaelimisha wananchi. Na mimi nitumie fursa hii kusema kwamba mnapoona kuwa waandishi wameandika ndivyo sivyo msiwatishie kuwafungia wala usalama wa maisha yao, ni vizuri mkawasahihisha kwamba walichoandika sio au ndio. Tuishi kwa amani!

Mheshimiwa rais wangu, ulipokuwa ukitimiza mwaka mmoja Ikulu nilikuandikia kuwa sidhani kama kuan mtu ambaye watanzania wa,ewahi kutokea kuwa na matumaini nae kama wewe. Sehemu ya makala hiyo ilikuwa hivi “
sina mengi ya kusema juu ya utawala wa Kikwete kwa siku 365, ninachoweza kusema ni kumtia moyo na kumpa ukweli kuwa akaze buti, hali bado ni rhumba kali. Safari bado ni ndefu! Nikiwa kama mzalendo wa nchi hii sina sababu ya kumpaka mafuta kwa mgongo wa chupa, nimeshuhudia watu wengi wanapoanza kuzungumzia utawala wa Kikwete mara hurejea kwenye hotupa zake na kwenye mikutano ya kampeni. Akiwa mgombea wa urais kupitia C.C.M Kikwete aliwakuna sana watanzania kwa ahadi zake kemkem. Ahadi hizo zilikua nzito na nzuri, akadiriki hata kusema wazi kuwa kama kuna ahadi ambazo atasahau basi ruksa kukumkumbusha.Aliwapa matumaini makubwa sana watanzania, mara nyingine ninaporudi nyuma kuangalia historia ya viongozi wa nchi hii najikuta namuonea huruma rais Kikwete. Namuonea huruma kutokana na ukweli kwamba je, asipotimiza ahadi hizo atawaeleza nini watanzania? Ni ahadi nzito na nyingi mno, huruma yangu inazidi nikiwaza ikiwa alitoa ahadi hizo ili apate kuingia Ikulu au kwamba kweli amedhamiria kuikwamua nchi hii.Unajua kwa nini nasema namuonea huruma? Watanzania ni miongoni mwa Waafrika wanaosota kimaisha kutokana na pengine sera mbovu za wanasiasa au ufisadi na ubinafsi wa viongozi wa nchi zao. Watanzania wamesubiri kwa hamu kubwa kiongozi kama Kikwete, ambaye anaweza akakiri tatizo hadharani bila kuficha wala kupamba kwa unafiki ili kuonekana kiongozi mzuri bila kujali kuwa anaua watu wake.

Watanzania hawajasahau dharau na ubabe wa viongozi wao kama ule wa Basil Mramba aliyekuwa waziri wa fedha katika serikali ya awamu ya tatu, chini ya Mzee Benjamin Mkapa, aliyeidhinisha ununuzi wa ndege ya rais kwa mabilioni ya shilingi huku nchi ikikabiliwa na janga la njaa.
Na mramba kwa jeuri kubwa akasema bora watanzania wale majani kuliko kuacha kununua ndege ya rais, eti watanzania wale majani? Kila ninapoikumbuka kauli hii, hushikwa na uchungu na machozi hunilenga. Hivi kweli Mramba alitudharau kiasi hiki watanzania? Sisi ambao nchi hii ni mali yetu na wala si wakimbizi au wavamizi. Anatusimanga katika nchi yetu wenyewe? Kwelii??Kidonda hiki cha wananchi hakijapona bado, kilitoneshwa zaidi pale waliposikia kuwa Mramba yuko tena ndani ya baraza la mawaziri, sio kila mtu alimwangalia vizuri Mramba ‘a.k.a’ ndege ya rais, tukadhani atajirekebisha.Baada ya muda tukasikia kuwa amemdanganya rais kuhusu ujenzi wa barabara ya shekilango na Sam Nujoma jijini Dar es salaam , kama hiyo haitoshi nasikia kule Mtwara au Lindi aliwahi kumkera hata waziri Mkuu, Mh. Lowassa”

Rais Kikwete nimeamua nikukumbushe tu kwamba nimeahi kuzungmza na wewe kupitia safu hii, kama wewe hujasoama basi kwa namna moja ama nyingine wasaidizi wako watakuwa walisoma.

Katika kukuambia nilichokusudia leo sina haja ya kuzunguka mbuyu au kufunika kombe mwanaharamu apite, ukweli ni kwamba watanzania walio wengi ukiondoa mawziri, wabunge, wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya wamekata tamaa, wamechoka!

Na sioni sababu ya kwa nini nisikuambie tu kwamba wanasema mitaani kuwa utawala wako umeanza kuwachosha watanzania. Lengo langu hapa sio kukuumiza wala kukudhihaki, nia yangu ni kukufanya uwe na taarifa hiyo ili uweze kuchukua hatua zinazostahili kunusuru hali, ndio maana nikasema nakusaidia, maana naamini kwamba ili kumsaidia rais, hainihitaji kuwa waziri au sehemu ya familia ya rais.

Miongoni mwa vitu ambavyo watanzania wanakatishwa tamaa ni kauli zako zinazoonekana wazi kumtetea mtangulizi wake bwana Mkapa katika tuhuma zinazomkabili, unavyoonekana mbele ya macho ya baadhi ya watanzania ni kwamba umeona kitu alichofanya Mkapa kuanzisha kampuni akiwa bado rais ni kitu kizuri na chenye kufaa, hii inatufanya tubaki njia pamnda katika ahadi yako ya kutofanya biashara Ikulu kama alivyofanya Mkapa.

Si hivyo, kuna maneno yanasemwa mitaani kwamba unamkinga Mkapa ili kwamba kama itatokea utafanya maovu ukiwa Ikulu basi atakayekufuata naye akukingie kifua kwa kisingizio cha kukucha upumzike. Hivi kweli ulithubutu kuwaziba midomo wasimhoji mwajiriwa wao mstaafu? Kuna ubaya gani kumhoji alichofanya ikiwa ni halali au la? Kama watanzania hawatamuhoji Mkapa, unataka nani amuhoji?

Binafsi mimi kijana wako nilishangazwa na misimamo yako mheshimiwa Rais, eti unataka Mkapa apumzike, sawa hatuna tatizo na Mkapa kupumzika, lakini nani atamjibia tuhuma hizo mzee Mkapa? Je ni Sumaye? Sumaye mwenyewe kasema kuna hoja alishindwa kuzijibu kwa makusudi kabisa kwa sababu hazina maana. Kama kuna uwezekano, ningekusihi kwamba uwaache wenye nchi wamhoji Mkapa, apumzike kwa kazi ipi? Mbona hajamaliza kulitumikia Taifa? Ikiwa ni pamoja na kutueleza alipataje mali anazomiliki sasa hivi? Mbona alipoingia alitaja mali? Kimya chake kwa kushindwa kutaja mali alizotuma ndicho kinachotutia mashaka kwamba Mkapa ana walakini!

Joseph Mbatia, mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi aliwahi kusema kwamba, ni hatari sana kuufikisha umma mahali pa kukata tamaa, hatuna lugha ya kutosha kukiri kuwa sasa watanzania wanaanza kukata tamaa.

Nikutie moyo rais wangu, kaza buti, anza wewe kujifunga mkanda, hali ni ngumu, macho ya mamilioni ya watanzania yako kwako, utawajibu nini watanzania utakapoondoka bila kutimiza zile ajira milioni moja, bila kudhibiti mfumuko wa bei, uhakika wa masikini kuwasomesha watoto wao vyuo vikuu, nasema utawajibu nini Watanzania?
Hivi ni kweli kwa kusoma magazeti na vyombo vingine vya habari hujagundua tu kuwa watanzania wamekata tamaa? Hujashtuka tu, najua sio rahisi wewe kufika kila kijiji cha Tanzania, kila wilaya nakadhalika, waliofika wanakwambia hali ni mbaya, fanya kila uwezalo ili matumaini ya Watanzania kwako yardi. Hii ni pamoja na kuwawajibisha wasaidizi wako ambao hawana msaada uwao wote katika kuwatumikia wananchi.

Sio mbaya kama ungeuliza nani hafai, mimi harakaharaka bila hata kuhitaji kufikiri ningekushauri umpumzishe Peter Msolla na wala sio Mkapa na wengine wanaofanana naye akiwamo Basil Mramba.

Nimejitoa kwa lolote, najua hawatafurahia ukweli huu, hata kama watakasirika na kufikia hatua ya kutaka hata kuniua, basi wakae wakijua kuwa nikifa Danieli kuna kina Daniel wengine wengi watazaliwa tena, hata hivyo hata kama wao hawataniua bado kuna siku moja nitakufa!

Mheshimiwa Rais, nakupenda ndio maana nakwambia watu wamekata tamaa! Ninakuombea, kwa hakika tuko nyuma yakom lakini kaa ukielewa kuwa kuna wasaidizi wako wanakuponza!

Mung ibariki Tanzania, bariki viongozi wake, wawe watu wa kukubali ukweli, wafanye kuelewa kua kukosolea si dhambi ya kuwapeleka jehanam! Amen!




Monday, June 18, 2007

TUKIAMUA KUWA WAZALENDO MTASTAHIMILI?

Ni rahisi sana kwa watawala wetu kama hawa wakisisitiza uzalendo kwa wananchi, kuna maswali kidogo nataka kuhoji hapa!

HIVI TUKIAMUA KUWA WAZALENDO, WANASIASA NA WATAWALA WETU WATASTAHIMILI?

.Je wanajua gharama ya uzalendo? Au wanasema tu?

Hala..hala wanasiasa mnapokuwa majukwaani. Jichungeni na kauli zenu. Muwe mnasema mnayomaanisha na kumaanisha haswa yale mnayoyasema!

Ndugu msomaji nimeamua nimejikuta nakuwa mkali tu leo, na si ajabu nikaitwa mbwatukaji, eti nabwatuka! Nambwatukia nani wakati mimi natoa elimu hapa? Nimeamua kuwa mkali kwa sababu sio siri kuna kauli na matamshi ya wanasiasa yanakera sana. Yanakera hasa unapozilinganisha kauli hizo na utendaji wake (wao?)

Hivi umewahi kuhudhuria mikutano, warsha, semina au nini zile…..? ‘Workshop’ za hasa wasemaji wakuu wanapokuwa wanasiasa? Hebu fikiria wito kama huu unaotolewa na huyu mheshimiwa nanihii…anasema “kwa hiyo nawaomba sana ndugu wananchi, muwe na moyo wa uzalendo kwa Taifa lenu” Mwingine najionyesha kuwa makini zaidi kwa kusema “unajua wakati umefika wa kuwa wazalendo” Msikilize na huyu anasema “eeeh!..uzalendo ni kitu muhimu sana kwa raia yeyote na wa taifa lolote kwa nchi yake”

Ni mahodari kweli wa kutoa matamko, kasheshe ni pale unapowadai watekeleze kauli zao kivitendo. Waambie waanzishe mitaala ya kufundisha uzalendo mashuleni, angau shule za chekechea tu, utapewa kila jina watakalojisikia kukupa au lile lililo rahisi kutamkwa na vinywa vyao.

Wengi wanato wito kwa wananchi kuwa wazalendo wakiwa hawajui gharama ya uzalendo pale wananchi wanapoamua kuwa wazalendo. Wanatunga mamba kwa hiari yao, lakini huwa wanakikimbia kile kinachozaliwa. Siwezi kuzungumza hapa leo ikiwa watanzania ni wazalendo au sivyo, isipokuwa, ukitaka kujua ukeli wa jambo hili angalia viongozi wa Tanzania, ung’amue ikiwa wao ni wazalendo au la!

Kwa ninavoelewa mimi uzalendo kwa lugha rahisi inayoweza kueleweka na kila mmoja ni hali ya kuwa na mapenzi ya dhati kwa nchi yake, si vibaya nikaongeza kwa kusema kuwa mtu mzaleno huwa tayari kujitoa mhanga kwa ajili ya Taifa lake, hasa pale linapohujumiwa bila kujali anayelihujumu ni nani na anatoka wapi!

Wanasiasa na watawala wanataka tuwe wazalendo, je watakuwa tayari kulipia gharama hii? Gharama ya watu hawa kujitoa mhanga kuijenga nchi yao? Nauliza hivi kwa sababu kuna mazingira yanaonesha kwamba watawala wengi hawapendi sana wananchi wawe na ufahamu wa kuelewa mwendo wa jinsi nchi yao inavyokwenda. Mwenendo wa watawala wao walivyo, ni haki yao maana waliwaweka madarakani, na mishahara yao ni kodi za wananchi!

Ngoja nitoe mawazo yangu hapa kuhusu wazalendo tunachoweza kukifanya tukishakuwa wazalendo. Mnatuambia tuwe wazalendo haya yafuatayo mtayaweza au ndio kule tunakodhani sisi watawaliwa ni janja ya maneno? Hata hivyo ikumbukwe kuwa kama wananchi hudhaniwa kuwa vikaragosi, wasiolewa mambo, mambumbu hawatabaki kuwa hivyo walivyo daima, kuna siku wataamka.

Uzalendo ambao wanasiasa wanatuhimiza sisi wenye nchi hii kuwa nao ni pamoja na kudai ahadi walizotuahidi wakati wa uchaguzi. Je watastahimili? Siku ambapo watakuwa wanapita na misafara ya utitiri wa magari yao kwenye majimbo yetu, watakubali tuwasimamishe, tuwaulize ahadi yao ya kutuletea maji jimboni iliyeyukia wapi na vipi? Watakubali tuwahimize kuwa muda unakwenda na hakuna lolote linalofanyika? Kusimamisha msafara jimboni tukiamua kuwa wazalendo haitakuwa na maana ya kuwakosea wakuu wetu adabu, itakuwa ni kujitoa mhanga wa kuwaonyesha kuwa tumeamua kuwa wazalendo na sio kuwa vikaragosi vya kuchezewa na kila mwanasiasa anayetaka ubunge jimboni kwetu.

Uzalendo ni pamoja na kuuliza inakuwaje mashirika yetu yanauzwa kwa bei ya kutupa? Ni pamoja na kuhoji kwa wanini viongozi wanakaa kimya wakati viwanda vyetu vinakufa nchini? Nani asiyejuwa kuwa vitu vingi vinaagizwa toka nje ili hali tunavyo hapa nchini? Kwa ninisamani ziagizwe nje ya nchi wakati tuna mininga, mikaratusi na aina zingine za miti inayoweza kutengeneza bidhaa hizo? Tukisema kuwa suala ni utandawazi, tutawahoji kuna ulazima gani wa kushikiria sera za mataifa ya magharibi huku tukijua kabisa kuwa zinapeperusha ndoto za maisha bora kwa kila mtanzania? Ni kweli hakuna la kufanya kulinda viwanda vyetu na wazalishaji wa ndani? Haya ni amswali ambayo watanzania wakiwa wazalendo watawauliza viongozi. Wanatuhimiza kuwa wazalendo, je haya watayastahimili? Je watatupa majibu yetu ya wazi na kweli? Je hawatatupachika majina na kutuita wenye wivu wa kike, wachochezi na kimbelembele? Maana huo ndio uzalendo!

Uzalendo ni pamoja na kuhoji juu ya uhalali wa viongozi kukingiana vifua hasa wanapokuwa na kashfa ikiwamo rushwa ambayo sasa hivi inaitwa uzembe kwa mujibu wa mwandishi Fulani hapa nchini. Tutawauliza kwa nini Fulani alifanya madudu haya halafu wewe unasema tumuache apumzike? Wasije juu na kutukunjia ndita, wasitukasirikie, wasitutishie maisha yetu na usalama wetu, maana huu ndio uzalendo! Hakuna maana ya kujiita wazalendo huku tukiiacha nchi ipelekwe na watu wachache kwa jinsi wanavyojisikia!

Uzalendo ni pamoja na kuhoji na kukemea ubadhirifu wa fedha za umma na baadhi ya viongozi wa ngazi tofauti tofauti. Na inapotokea hivyo wasituite majina wanayojisikia kutita, kama wana haja ya kutuita kwa majina yetu basi watuite yale majina halisi tuliyopewa na wazazi utotoni. Maana hii ndio gharama ya uzalendo!


Uzalendo una mengi, na mengi hayo hayapendwi na watawala, huu ndio ukweli! Wanapotuhimize uzalendo kwa wananchi, ikiwa si wanafiki waanze wao kuwa wazalendo, kwa kuacha kuhujumu taifa hili kwa wale wanaofanya hivyo, maana hata serikali inakiri kuwa kuna wahujumu, kwa mfano wale watendaji wanaotumia fedha za serikali (zetu) vibaya! Ikiwezekana pia wapunguze bei za katiba ya nchi yetu ili kila mtu amudu kununua, kasha maduka ya serikali yafunguliwe kila mahali ili hata watanzania wa vijijini wanunue wasome wawe na vigezo (grounds) za kuwakosoa na kuwakosoa au kuwapongeza na kuwakumbusha inapobidi!

Kuuliza hivi ikiwa watamudu gharama za uzalendo au la haina maana kuwa wakikataa gaharama hizo hatutakuwa wazalendo, hata wakikataa na kuacha kuhimiza uzalendo, bado tutaamshana ili tuwe wazalendo!

Mungu ibariki Tanzania, Mungu bariki watanzania!



Friday, June 15, 2007

Hali ni mbaya, nimeona leo tushirikishane juu ya uzalendo! Uzalendo! Unajua uzalendo wewe? Hali ya kujitoa kuipenda nchi yako, unaithamini, unailinda kimaadili, kisiasa, kiitikadi na kadhalika. Nasema unaipenda nchi yako, huu unaitwa uzalendo, naam kuipenda nchi yako.

Utashangaa nikikwambia kwamba binadamu wengi (sio wote) waishio katika nchi ya Tanzania, hawaipendi Tanzania. Nimesema binadamu, nimeogopa kutumia neno ‘watanzania’ Unaweza usinielewe. Labda niseme hivi, Watanzania (kama ulivyozoea kuita) wengi hawana mapenzi na nchi yao. Wako tayari kufanya lolote baya na kuidhuru nchi yao.

Hii ni kuanzia viongozi wa nchi mpaka raia wa kawaida. Hawaitaki Tanzania wala vilivyomo humu. Namaanisha kwamba, hawapendi lugha yao ya Kiswahili, wananchi wenzao, viongozi wao, mavazi yao( vazi la Tanzania ni lipi?) Unaweza kunizodoa kwa hoja hiyo. Nitakuuliza swali, ule mpango wa kubuni vazi la taifa umeishia wapi? Liko wapi hilo vazi? Juhudi zipi zimefanywa na wizara yenye dhamana ya utamaduni wa nchi hii kuhamasisha matumizi ya vazi hilo? Umewahi kumuona waziri wa utamaduni wa nchi hii amevaa vazi la kitanzania? Uliona waziri wa utamaduni siku alipokuwa akiapishwa alivaa vazi la wapi? Hiyo kazi nakupa katafute jibu, kama ukijisikia nitumie jibu hilo.

Tuhamie kwa wabunge wetu, wanapokuwa na vikao vyao kule Dodoma, si umewahi kusikia, huwa wanageuka na kuwa waingereza? Hawataki kutumia lugha yao ya Taifa, wanasahau kabisa kwamba wao ni wawakilishi wa mamilioni ya Watanzania ambao hawajui lugha hiyo ya kiingereza. Tatizo lao ni nini? Kwa nini wasitumie lugha yao asili ambayo pamoja na kuzungumza pia ni kuikuza ili iwe ya kimataifa kama ilivyo kwa lugha ya kiingereza? Huu ni uzalendo?

Waangalie nao wasomi wetu, wanaandaa mada zao wakiwalenga watanzania, bado wanatumia kizungu kuwasilisha mada hizo, sijui kama watakupa sababu za kueleweka zinazowafanya wakwepe kutumia Kiswahili utakapowataka wafanye hivyo. Je huu ni uzalendo?

Tusafiri pamoja na kufika kwenye asasi mbalimbali, kule kwa wanaotumia kiingereza wanaita NGO’s, asasi hizi ni zile zenye waasisi wa kitanzania. Ziwe za kuhusu elimu ya UKIMWI, elimu, afya na kadhalika. Wanapoweka matangazo yao, angalia kwa makini, mengi yako kwa lugha ya kiingereza kana kwamba wanawasiliana na watu wa mataifa mengine ambayo si Tanzania, kazi tunayo!

Tusiache kuwatembelea vijana vijiweni, hawa ndio kabisa, siku hizi ili waonekane bora watakwambia wanazungumza kizungu, wanacheka kizungu, wanavaa kizungu (vitovu vikiwa nje kwa upande wa mabinti) n.k hawataki kuonekana kuwa ni watanzania.

Unajua nini namaanisha katika makala hii? Chochote unachofanya ili kuihujumu nchi yako kwa namna yoyote ile, tunasema huo si uzalendo. Nimetoa mfano mdogo tu wa kuidharau lugha yetu.

Je nimetoka nje ya mada? Hivi nazungumzia nini hapa? nazungunzia nini vile? Aah!..nimekumbuka, nilikuwa nahoji sababu ya wasomi kusota mitaani wakiwa taabani kiuchumi. Nikasema tatizo ni uzalendo.

Maana yangu ni hii, viongozi wa nchi hii wamekuwa si wazalendo, utendaji wao unathibitisha hilo. Kama kiongozi ni mbovu na anashutimiwa wazi wazi kwa rushwa na hataki kujiuzulu, tumwiteje kama si mtu wa kuihujumu nchi yetu?

Mtu anayeingia mikataba ya siri ambayo baadaye inasababisha mahangaiko kwa wananchi wake tumpe jina gani? Au mtu anayeiuza nchi kwa kisingizio cha ubinafsishaji (usio na mpangilio) tumbatize jina lipi? Nisaidieni tafdhali!

Mtu anayeuza mashirika ya umma na kuwapa wazungu kwa kigezo cha kuboresha uzalishaji na kukuza uchumi wa nchi hii apewe jina gani? Ni wahujumu hawa!

Naomba niongeze swali hapa, nitafutieni jina la kumpa mtu anayewanyima mikopo wanafunzi kwa kisingizio cha alama za kufaulu, huku akijua wazi kuwa anarudisha nyuma maendeleo ya elimu yetu nchini. Mimi namwita mhujumu wa elimu ya nchi hii, hivyo si mzalendo!

Viongozi wengi wa nchi, huwa wanajisahau wanapoyakwaa madaraka, ndani Yao huzaliwa kitu kinaitwa ubinafsi, hawataki tena kujishughulisha kitaifa, pengine hujishughulisha zaidi na familia zao na jamaa zao. Kama ndivyo napata swali, kwa nini waliyakubali madaraka, kwani hawakujua kuwa wanakwenda kuwatumikia wananchi na si familia zao?

Wajibu wa kuandaa mazingira ya ajira na kujiajiri ni wa serikali. Serikali ndio inayoweka kanuni na taratibu za ajira na kujiajiri. Wananchi hata kama wangekuwa na uwezo wa kujiajiri, bado watalazimika kufuata taratibu na kanuni zilizowekwa na serikali yao. Sera na mipango.

Uzalendo…uzalendo uzalendo, naimba wimbo huu uzalendo, nasisitiza uzalendo. Hata hivyo ni muhimu kufahamu kuwa kuamua kua mzalendo kwataka moyo, kuna gharama za kuwa mzalendo na ndio maana huwa naamini kuwa uzalendo sio tabia, na kama ni tabia basi ni ile tabia sugu, imebadilika inakuwa ‘spirit'

Umeelewa hoja yangu ya leo, basi amka twende!
0713 550 778


Monday, June 11, 2007

SINZA INATIA AIBU KWA UCHAFU!

Huu ni moja tu kati ya mitaa michafu ya kule kunakoitwa Sinza kwa wajanja! Huu ni mtaa maarufu wa Sinza Msikitini au, wakazi wanapita kwenda maofisini, sidhani hata kama kuna mtu mmoja anawaza cha kufanya!